Na Mwandishi Wetu
NAIBU Katibu Mkuu wa Wizara ya Uhusiano wa Kimataifa na Ushirikiano ya Afrika Kusini, Balozi Tebogo Seokolo, amezihimiza Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuchukua hatua madhubuti za kukuza zaidi mtangamano wa kikanda,
Kwa kuongeza kiwango cha biashara baina ya nchi hizo kutoka kiwango cha sasa cha asilimia 23.
Ametoa wito huo wakati wa Mkutano wa Kamati ya Makatibu Wakuu wa SADC ulioanza jijini Pretoria, Afrika Kusini, leo Machi 7, 2026, chini ya uenyekiti wake.

Katika hotuba yake, Balozi Seokolo amesisitiza umuhimu wa Nchi Wanachama kuimarisha sekta ya viwanda, akibainisha kuwa sekta hiyo inaendelea kukua kwa kasi na kwa sasa inachangia takribani asilimia 11 ya pato la ndani (GDP) la nchi za SADC.
Aidha, ameeleza umuhimu wa kuboresha miundombinu, hususan barabara, ili kurahisisha usafirishaji, mwingiliano wa watu na biashara ndani ya kanda.
Pia amesisitiza umuhimu wa kuimarisha usalama wa chakula na lishe, akieleza kuwa takribani watu milioni 58 katika kanda ya SADC wanakabiliwa na changamoto ya uhakika wa chakula.

Kwa upande wake, Kiongozi wa Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Said Shaib Mussa, ameeleza hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha maeneo hayo kwa kushirikiana na Nchi Wanachama wa SADC.








