Na Lucy Lyatuu, Dodoma
TUME Ya Taifa Ya Mipango (NPC) kesho jumatatu Februari 2,2026 itawasilisha nyenzo kuu tatu kwa Bunge La Jamhuri Ya Muungano zitakazowezesha kuanza utekelezaji wa Dira 2050.
Aidha Bunge linatakiwa kupokea, kujadili kwa wiki nzima na kufanya uamuzi kwa mujibu wa Katiba.
Nyenzo hizo ni pamoja na mpango elekezi wa muda mrefu yaani wa miaka 25 kuanzia mwaka 2026/2027 hadi mwaka 20250/2051 na Mpango elekezi wa miaka mitano kuanzia mwaka 2026/2027-2030/2031.
Nyenzo nyingine ni mapendekezo ya mpango wa maendeleo ya Taifa wa mwaka 2026/2027 ambazo zitawasilishwa na serikali kupitia Waziri wa Nchi (Mipango na Uwekezaji) Profesa Kitila Mkumbo.
Katibu Mtendaji wa Tume hiyo, Dkt Fred Msemwa amesema hayo jijini hapa wakati akitoa taarifa kwa umma kuhusu maandalizi ya kuanza kwa utekelezaji wa Dira 2050.
Amesema mipango hiyo imepitia ngazi zote za uamuzi serikalini, ambapo itawasilishwa ili kutoa nafasi kwa Bunge kujadili na baadae kufanya maamuzi.
Dkt Msemwa amesema pamoja na nyenzo hizo, Tume imeandaa muongozo utakaohakikisha Mamlaka za serikali za mitaa yakiwemo majiji na Manispaa zote, mikoa yote, Taasisi za umma na Idara na Wizara mbalimbali zinaongozwa vizuri katika kutafsiri na kuelewa mataraji ya Dira 2050 kwa usahihi.
“Kwa msingi huo NPC imeandaa Muongozo wa upangaji wa mipango ya Taifa, ” Amesema Dkt Msemwa na kuongeza kuwa katika kuhakikisba kuwa Muongozo huo unaeleweka baina ya wadau NPC imeshafanya semina na viongozi kutoka Halmashauri zote, Wizara, Idara na Taasisi za umma ili kujadili muongozo huo na kuwa na uelewa wa pamoja.
Amesema katila hatua nyingine NPC ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha mfumo wa kielektroniki wa ufuatiliaji wa tathmini unaolenga kuleta mageuzi ya ufuatiliaji unaozingatia zaidi matokeo ya kazi nanuwajibikaji ambao utaanza kutumika pamoja nanutekelezaji wa Dira 2050 ifikapo Julai 2026.
Kuhusu wananchi kufuatilia uwasilishwaji wa nyenzo hizo, Dkt Msemwa amesema ni muhimu kwa kuwa Dira 2050 imebeba matumaini ya Watanzania na imeandikwa kuzingatia maoni yao, hivyo ni muhimu wananchi kujua na kufuatilia mipango iliyoandaliwa ili kutekeleza Dira yao.
Amesema pia ni fursa ya pekee kwa kila mwananchi kwa kuwa uwasilishwaji wake ni jambo lisilotokea mara kwa mara kwani utatokea tena baada ya miaka 25 ijayo, hivyo ni muhimu wananchi kufuatilia mustakabli wa Taifa lao.
” Dira inasisitiza kuhusu ustawi wa pamoja na ushiriki wa kila mmoja katika ujenzi wa Taifa, Dira ni alama ya umoja na ina nia thabiti ya kutomuacha yeyote nyuma hivyo ni muhimu kila mtanzania kuwa na taarifa kamili ya kinachoendelea katika Mipango ya maendeleo ya Taifa, ” Amesema.

