Na Lucy Ngowi
MBUNGE wa Kasulu Mjini, Profesa Joyce Ndalichako, ameiuliza Serikali kuhusu mpango wake wa kuanza utekelezaji wa mradi wa usambazaji maji katika eneo la Mwanga B, jimboni humo.
Profesa Ndalichako alihoji swali hilo bungeni jijini Dodoma, akitaka kujua lini mradi huo utaanza rasmi.
“Je, Serikali itaanza kutekeleza Mradi wa Usambazaji Maji Mwanga B katika Jimbo langu la Kasulu?” alihoji mbunge huyo.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Maji, Mathew Kundo, alisema Serikali tayari imeanza utekelezaji wa mradi huo uliopo mjini Kasulu, mkoani Kigoma.
Kundo aliongeza kuwa mkandarasi wa mradi tayari amesambaza mabomba yote yenye urefu wa kilometa 52 katika eneo hilo.
Aidha, kazi nyingine zinazotarajiwa ni pamoja na kubadili mfumo wa nishati kutoka jua kwenda gridi ya umeme kwa ajili ya uzalishaji wa maji, pamoja na ujenzi wa chemba za ukaguzi wa mtandao wa mabomba.
“Mheshimiwa Spika, mradi huu utakapokamilika unatarajiwa kunufaisha wananchi 68,000 wa mitaa sita ya Mwanga B, Muganza, Msambara, Nyachidima, Kimwobwa na Kigondo,” alisema Kundo.
Aliongeza kuwa Serikali itahakikisha inapeleka fedha za kutosha kwa ajili ya mradi huo ili ukamilike na kuanza kutoa huduma ya maji kwa wananchi waliokusudiwa kufaidika.

