Lucy Ngowi
DODOMA: WAZIRI wa Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, ameiagiza Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) kutoa adhabu kali kwa madereva na makondakta watakaobainika kuwanyanyasa wanafunzi.
Profesa Mbarawa alitoa agizo hilo leo Februari 4, 2026, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu kuboresha usafiri wa wanafunzi katika miji.
Amesema LATRA inapaswa kuhakikisha madereva na makondakta wote wanathibitishwa na kusajiliwa, huku wakidhibiti nauli, staha ya huduma, na usalama wa wanafunzi kwa wakati wote.
Pia alisisitiza kutoa elimu kwa watoa huduma ili wafuate haki na wajibu wao.

Aidha, Wizara ya Uchukuzi imeagiza ziwepo namba za bure kwenye treni za abiria, daladala, na mabasi yaendayo mikoani na nchi jirani ili abiria waweze kuripoti malalamiko kwa urahisi.
Profesa Mbarawa pia aliagiza kushirikiana na Jeshi la Polisi kufanya ukaguzi wa mara kwa mara na wa kushtukiza katika vituo vya daladala, hasa nyakati za asubuhi na jioni.
Agizo hilo limekuja baada ya video iliyosambaa mitandaoni ikionyesha binti Mariana Mirindima, mwanafunzi wa kidato cha kwanza Shule ya Sekondari Jangwani, akiwasilisha barua inayoripoti changamoto wanazokutana nazo wanafunzi.
Katika barua yake, Mariana alieleza kuwa makondakta wanagoma kuwabeba wanafunzi wakidai kuwa hawalipi nauli kamili, hali inayowalazimisha kusubiri muda mrefu njiani, kuchelewa shuleni, na kukosa usalama.
Mwanafunzi huyo aliomba wizara ichukue hatua stahiki dhidi ya watoa huduma wa daladala ili kuhakikisha wanafunzi wanapata haki yao ya msingi ya elimu na usafiri salama.

