Na Mwandishi Wetu
WATAALAMU wa masuala ya fedha na bajeti kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamekutana jijini Pretoria, Afrika Kusini kujadili hali ya kifedha ya jumuiya hiyo pamoja na mikakati ya kuongeza vyanzo vya mapato kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo ya kikanda.
Kikao hicho cha Kamati ya Fedha cha SADC kinafanyika leo Machi 9, 2026 na kinahusisha wawakilishi wa nchi wanachama, akiwemo Kamishna wa Fedha za Nje kutoka Wizara ya Fedha Tanzania, Rishade Bade, anayeongoza ujumbe wa wataalamu wa Tanzania.
Katika kikao hicho, wajumbe wanajadili hali ya michango ya nchi wanachama wa SADC pamoja na mapitio ya utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2025/26 kwa kipindi cha miezi tisa kuanzia Aprili hadi Desemba 2025.

Pia wanapitia mapendekezo ya bajeti ya jumuiya hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/27 pamoja na makadirio ya mapato na matumizi ya SADC kwa kipindi cha muda wa kati kuanzia mwaka 2027/28 hadi 2030/31.
Aidha, wataalamu hao wanajadili kwa kina mikakati ya kuongeza rasilimali fedha kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo ya kikanda, pamoja na utekelezaji wa uanzishwaji wa Mfuko wa Maendeleo wa Kanda.

Taarifa zinaeleza kuwa nchi 11 kati ya 16 wanachama wa SADC, ikiwemo Tanzania, tayari zimesaini mkataba wa kuanzishwa kwa mfuko huo ambao unatarajiwa kuwa chanzo muhimu cha fedha kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo katika kanda hiyo.
Kikao cha Kamati ya Fedha ni miongoni mwa vikao vya maandalizi kuelekea Mkutano wa 47 wa Baraza la Mawaziri wa SADC utakaofanyika Machi 12 na 13, 2026.




