Na Danson Kaijage
DODOMA: NAIBU Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile ametoa wito kwa wananchi kutowachagua wagombea wanaomba nafasi hizo kwa kutoa rushwa.
Amesema hayo alipotembelea banda la Mamlaka ya kupambana na kuzuia Rushwa TAKUKURU wakati wa maonesho ya wiki ya Utumishi katika viwanja vya chinangali Park Jijini Dodoma.

Amesema Serikali haitavumilia miradi yoyote inayoisimamia iwapo itabainika kuwa na viashiria vya rushwa.
Amesema ni jukumu la TAKUKURU kuhakikisha nidhamu ya fedha inazingatiwa kikamilifu hususani katika kipilmdi cha kuelekea uchaguzi mkuu.
Pia amesema uwazi na uwajibikaji ni nguzo muhimu katika kuhakikisha rasilimali za umma zinatumika kwa tija na kwa faida ya wananchi wote, huku akiwataka watumishi wa umma kuendelea kuwa mstari wa mbele katika kulinda maslahi ya taifa.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Uelimishaji Umma – TAKUKURU Mkoa wa Dodoma, Faustine Malecha, amesema taasisi hiyo inatumia maonesho hayo kuelimisha jamii kuhusu athari za rushwa kwenye uchaguzi na utekelezaji wa miradi ya umma.

“Tunahakikisha wananchi wanajengewa uelewa juu ya haki yao ya msingi ya kuchagua viongozi bora bila kushawishiwa kwa rushwa, kwani chaguo la viongozi kwa misingi ya hongo hudhoofisha maendeleo ya jamii nzima,” amesema.
Amesisitiza kuwa Taasisi yake imejipanga kusimamia nidhamu ya matumizi ya fedha za umma kwa karibu zaidi, ili kuhakikisha miradi ya maendeleo haigeuki kuwa mwanya wa kujipatia utajiri wa haramu.
“Tutashirikiana na Wananchi kuhakikisha kuwa kila hatua ya utekelezaji wa miradi inazingatia sheria, kanuni na maslahi ya taifa,” amesema