Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: RAIS wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Februari 8, 2026 amefungua rasmi Soko Kuu Jipya la Kariakoo jijini Dar es Salaam, akisisitiza kuwa mradi huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha mazingira ya biashara, kuongeza tija ya uchumi na kulinda mitaji ya wafanyabiashara.
Rais Dkt. Samia amesema ujenzi wa soko hilo ni matokeo ya dhamira ya Serikali ya kurejesha Soko la Kariakoo baada ya soko la awali kuteketea kwa moto Julai 2021, kwa kufanya ukarabati na kujenga soko jipya linalokidhi viwango vya usalama, ubora na mahitaji ya biashara ya kisasa.
Amehimiza uendeshaji wa soko hilo kuzingatia misingi ya ufanisi, nidhamu na ushindani wa haki, akibainisha kuwa Kariakoo ni mhimili wa biashara ya kitaifa na kikanda, na kitovu muhimu cha uchumi kinachowaunganisha wazalishaji, wasambazaji, wauzaji na wanunuzi kutoka ndani na nje ya nchi.
Vilevile, Rais Dkt. Samia ameipongeza Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), makandarasi na wasimamizi wa mradi kwa kujenga miundombinu yenye ubora wa hali ya juu, ikiwemo mifumo ya usalama na huduma za kijamii.
Ameuelekeza uongozi wa soko kuendelea kuimarisha mazingira rafiki kwa wanawake wafanyabiashara, ikiwemo huduma za mama na mtoto.
Katika kuhakikisha uendeshaji wenye tija, Rais Dkt. Samia amesisitiza umuhimu wa mifumo thabiti ya zimamoto, uokoaji na dharura, pamoja na upangaji rasmi wa ratiba za kushusha na kupakia mizigo ili kupunguza msongamano na kurahisisha biashara.
Akihitimisha, Rais Dkt. Samia amesema Soko Kuu Jipya la Kariakoo ni uwekezaji wa kimkakati wa Taifa unaopaswa kulindwa na kusimamiwa kwa ufanisi, ili liendelee kuwa injini ya uchumi na mfano wa masoko ya kisasa barani Afrika.

