Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Profesa Mohamed Sheikh Akagua Gati la Kuegeshea Meli la Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO)
Na Lucy Ngowi
SERIKALI imeanza utekelezaji wa mpango wa kimkakati wa kuibadilisha sekta ya uvuvi nchini, ikilenga kuifanya kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi.
Mpango huo unajumuisha ununuzi wa meli za uvuvi wa bahari kuu, upanuzi wa ufugaji wa viumbe wa maji, na ujenzi wa miundombinu ya kisasa ya uvuvi.
Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia sekta ya uvuvi, Profesa Mohamed Sheikh, alisema serikali tayari imenunua meli moja ya uvuvi ambayo ipo katika maji ya Tanzania na itaanza shughuli zake mara baada ya kukamilika kwa taratibu za mwisho.
Aidha, meli nyingine nne ziko katika hatua mbalimbali za manunuzi ili kuongeza uzalishaji wa samaki katika bahari kuu.
Profesa Sheikh alisema uwekezaji huu ni sehemu ya dira ya dhati ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuibadilisha sekta ya uvuvi kutoka kujikimu hadi kuwa sekta yenye uzalishaji mkubwa, itakayochangia ukuaji wa uchumi na kuongeza mapato ya kigeni.
Kwa sasa sekta ya uvuvi inachangia takribani asilimia 1.8 ya Pato la Taifa, lakini serikali inalenga kuongeza mchango huo hadi angalau asilimia 10 ifikapo mwaka 2030.
Moja ya mikakati muhimu ni kuendeleza ufugaji wa samaki, ambavyo kwa sasa vinachangia takribani asilimia 7 ya uzalishaji wa samaki, huku asilimia 93 ikitokana na uvuvi wa asili unaokabiliwa na changamoto kama uvuvi haramu, ongezeko la idadi ya watu, na mabadiliko ya tabianchi.
Serikali inalenga pia kuzalisha vifaranga bora vya samaki, kuongeza aina za samaki zinazofugwa, na kuvutia wawekezaji.
Tanzania ina eneo la bahari lenye kilomita za mraba 223,000, sawa na asilimia 45 ya ukubwa wa nchi.
Kutumia rasilimali hii kikamilifu kutasaidia kuongeza uzalishaji wa samaki, kukuza uchumi, na kuboresha lishe ya wananchi.
Pia, ujenzi wa bandari za kisasa za uvuvi Kilwa Masoko na Bagamoyo unatarajiwa kuongeza uwezo wa huduma katika sekta hii.
Profesa Sheikh alibainisha kuwa uwekezaji huu utasaidia kuimarisha Shirika la Uvuvi Tanzania (TAFICO), kuhakikisha meli za taifa zinamilikiwa na kuendeshwa, kupunguza utegemezi wa meli za kigeni, na kuhakikisha mapato yanazunguka ndani ya nchi.

