NA MWANDISHI WETU, DODOMA
MAKAMU wa Rais, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, amezitaka wizara zinazohusika na masuala ya mazingira kuongeza juhudi katika kulinda na kuhifadhi mazingira ili Tanzania iwe mfano bora katika uhifadhi endelevu.
Amesema nchi ina rasilimali za misitu pamoja na wataalamu wenye uwezo wa kutosha kufanikisha malengo ya kulinda mazingira.

Dkt. Nchimbi ametoa kauli hiyo alipokutana na viongozi mbalimbali wa serikali akiwemo Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Masauni na Naibu Waziri wa Maji, Kundo Mathew.
Wengine ni Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Festo Dugange pamoja na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Richard Muyungi.
Kikao hicho kilihusisha pia wataalamu kutoka wizara hizo na kilifanyika jijini Dodoma.

Katika mazungumzo hayo, Makamu wa Rais amesisitiza umuhimu wa wizara hizo kushirikiana kwa karibu na kuandaa mpango wa pamoja utakaosaidia kulinda mazingira kwa ufanisi zaidi.
Ameeleza kuwa sekta nyingi zinazohusiana na mazingira hutegemea sana uhifadhi wa misitu na rasilimali asili ili kufanikisha majukumu yake.
Ametolea mfano kuwa Wizara ya Maji haiwezi kufanikisha kazi zake ipasavyo ikiwa vyanzo vya maji vitaharibiwa, huku matumizi ya nishati safi ya kupikia yakisaidia kupunguza ukataji holela wa miti.
Aidha, Dkt. Nchimbi amewataka watendaji kuongeza juhudi katika kutekeleza mpango wa kitaifa wa upandaji miti, unaoendana na juhudi za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa akihamasisha wananchi kupanda miti mara kwa mara, ikiwemo katika maadhimisho ya siku yake ya kuzaliwa.
Pia amewataka viongozi hao kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha miti inayopandwa inalindwa na kutunzwa ili kufikia malengo ya kuhifadhi mazingira.

