Na Danson Kaijage
DODOMA: RAIS Samia Suluhu Hassan amesema Jiji la Dodoma kwa sasa litakuwa jiji la kitalii, ikiwa ni pamoja na kuongeza kipato cha mtu moja mmoja kutokana na fursa zinazoendelea.

Samia amesema hayo alipowahutubia wananchi wa jiji la Dodoma na viunga vyake katika eneo la Nala muda mfupi baada ya kumaliza ukaguzi wa ujenzoi wa barabara ya mzunguko wa nje na uwanja wa ndege wa msalato ambao ni uwanja mkubwa na wa kisasa.
Kabla ya kuhutubia wananchi hao, Samia na Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dkt. Akinwumi Adesina, walifanya ukaguzi wa miradi hiyo na kuridhishwa na kuridhishwa nayo.

Hivyo Rais Samia ameziagiza Wizara ya ujenzi na ya Uchukuzi kuhakikisha kazi za ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya barabara, reli na viwanja vya ndege zinatekelezwa kwa viwango vinavyotakiwa.
Pia ameagiza kupandwa mazao mbalimbali ikiwemo zabibu ili kuendeleza asili ya maeneo hayo.
Kuhusu gharama amesema, barabara ya mzunguko wa nje ya Jiji la Dodoma imetumika Sh. Bilioni 489.892 ambapo serikali imechangia asilimia 15 katika fedha hizo.
Kwa upande wa ujenzi wa uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato, umegharimu Sh. Bilioni 370 hadi kukamilika kwake ukiwa na uwezo wa kubeba abiria milioni 1.5 kwa mwaka ikiwa ni kiwango Cha kitaifa cha daraja la 4F

Samia ameridhia ombi lililotolewa na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega lakutaka barabara ya mzunguko wa nje ya jiji la Dodoma, kuitwa jina la Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Akinwumi Adeshina.
Kwa upande wake Waziri wa ujenzi, Ulega amesema barabara ya mzunguko ya nje ya jiji la Dodoma aliyoikagua Rais Samia itaepusha foleni katikati ya jiji na kurahisisha huduma mbalimbali ikiwemo kusafirisha mazao.

Naye Dkt. Adesina ameeleza bayana kwamba Dodoma sasa ni mji wa kivutio barani Afrika.

Juzi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), kilimtunuku Dkt. Adesina Shahada ya Heshima ya Sayansi kutokana na benki hiyo kutoa mchango mkubwa kwa jamii na taifa nchini Tanzania.