Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) imesema kuwa Serikali imefanikiwa kuratibu na kuwezesha usajili wa makampuni 408 ya Kitanzania kuruhusiwa kusafirisha mazao mbalimbali ya kilimo kwenda soko la China.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na mamlaka hiyo, mafanikio hayo yamepatikana kupitia ushirikiano kati ya Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Ubalozi wa Tanzania nchini China pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China.
Makampuni hayo yamesajiliwa rasmi katika mfumo wa Mamlaka Kuu ya Forodha ya China, huku orodha ya makampuni husika ikiambatanishwa na taarifa hiyo.
TPHPA imeeleza kuwa usajili huo ni sehemu ya utekelezaji wa masharti ya Afya na Usalama wa Mimea na Chakula pamoja na makubaliano ya kibiashara kati ya Tanzania na China.
Lengo ni kuhakikisha kuwa mazao ya kilimo yanayosafirishwa kwenda nchini humo yanakidhi viwango vya afya ya mimea, ubora na usalama wa chakula vinavyotakiwa na soko la China.
Mamlaka imewakumbusha makampuni yote yaliyosajiliwa kuendelea kuzingatia kikamilifu masharti ya usimamizi wa afya ya mimea, ufuatiliaji wa mazao, matumizi sahihi ya viuatilifu pamoja na taratibu zote za ukaguzi kabla ya usafirishaji.
Aidha, TPHPA imetoa wito kwa makampuni mengine yanayopenda kusafirisha mazao ya kilimo kwenda China kuwasilisha maombi yao kupitia Mamlaka hiyo kwa ajili ya kupatiwa mwongozo wa taratibu za kuingia katika soko la China kupitia mfumo wa GACC.
Vilevile, Mamlaka imewahimiza wadau wote wa sekta ya kilimo na biashara kuendelea kushirikiana na kuzingatia sheria, kanuni na miongozo iliyopo ili Tanzania inufaike kikamilifu na fursa kubwa ya soko la China.
Soko hilo linatarajiwa kuongeza mauzo ya mazao ya kilimo nje ya nchi, kukuza uchumi wa wakulima na kuchangia pato la taifa.
TPHPA imesisitiza kuwa itaendelea kufanya ukaguzi na ufuatiliaji wa mara kwa mara ili kuhakikisha masharti ya kitaifa na ya nchi lengwa yanazingatiwa ipasavyo.
TPHPA imetoa shukrani kwa uongozi wa Wizara ya Kilimo kwa kuiwezesha Mamlaka kufanikisha upatikanaji wa soko la China.
Aidha, Mamlaka imeahidi kuendelea kufungua masoko ya bidhaa za kilimo katika nchi nyingine duniani, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika utekelezaji wa Ajenda ya 10/30 ya Wizara ya Kilimo.

