Na Lucy Ngowi
ASUBUHI inapopambazuka katika eneo la Zuzu jijini Dodoma, mwanamke Beatrice Julius huamka, huandaa mambo ya nyumbani, kisha kuelekea kwenye eneo analofanyia biashara yake ya matunda.
Hapa ndipo maisha ya kawaida yanavyokutana na ushupavu wa wanawake wanaotafuta riziki.
Kati yao, anasimama mwanamke mwenye tabasamu la matumaini, anayesukuma mkokoteni wa matunda na kufanya biashara katika eneo la General, Dodoma.
Huyu ni Beatrice, mama na mfanyabiashara ambaye kwa miaka mitano sasa amejitahidi kujenga maisha bora ya familia yake kupitia biashara ya matunda.

Beatrice ni mama wa watoto wanne na mkazi wa Zuzu, lakini biashara yake anaifanya kila siku katika mkokoteni eneo la General.
Akisimulia jinsi alivyoanza biashara yake anasema,
“Nilianza na mtaji kidogo sana, lakini polepole nikaanza kuzoea biashara. Huu ni mwaka wa tano sasa tangu nianze kuuza matunda.”
Mkokoteni wake hujazwa parachichi, ndizi mbivu na machungwa yanayovutia wateja.
Hata hivyo, kama wafanyabiashara wengi wadogo, Beatrice anakabiliwa na changamoto nyingi, hasa mabadiliko ya misimu ya matunda na mtaji unaoyumba.
“Kuna muda mwingine mtaji unayumba na mwingine unakaa sawa. Ukikaa sawa unaweza kujaza mkokoteni mzima na matunda mengi zaidi,” anaeleza.

Kwa mujibu wa TAMWA wanawake wafanyabiashara wadogo wana mchango mkubwa katika uchumi wa familia na jamii.
TAMWA inasema,
“Wanawake wafanyabiashara ndogo ndogo wanaojihusisha na biashara ndogo ni nguzo ya maendeleo ya familia.
Wanapaswa kupewa fursa sawa, msaada wa kibiashara, na ulinzi sokoni ili kuweza kuendeleza biashara zao kwa usalama” (Chanzo: TAMWA, 2025).

Akizungumzia zaidi juhudi hizo, Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Rose Reuben, anasema wamekuwa wakishirikiana na kina mama mboga mboga kama sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Mwanamke, ambapo hupata nafasi ya kusikiliza changamoto zao moja kwa moja.
Maadhimisho ya siku ya wanawake hufanyika kila mwaka Machi 8.
Anasema wamebaini kuwa wanawake hao wanakutana na changamoto nyingi, ikiwemo ugumu wa kufuata bidhaa zao asubuhi kutokana na ukosefu wa usalama, vitendo vya wizi, pamoja na wakati mwingine bidhaa zao kutonunuliwa kwa wakati.
Aidha, anasema TAMWA imekuwa ikitoa elimu ya namna ya kukuza mitaji na kuwaunganisha na taasisi za kifedha ikiwemo CRDB Bank, hatua ambayo imepokelewa vizuri na kina mama hao kwa kuwa inawasaidia kufanya uamuzi sahihi wa kibiashara kwa wakati.
Pia anasema wajasiriamali hao wamefurahia elimu hiyo kwa sababu inawasaidia kutoa uamuzi sahihi kwa wakati muafaka.
Vilevile, Dkt. Rose anasema katika kongamano hilo wanawake wamezungumzia ukatili wa kijinsia wanaokutana nao, kuanzia wanapofuata bidhaa zao hadi wanapokuwa sokoni na hata katika mazingira ya familia, ambapo wamejifunza namna ya kutafuta suluhisho na kujilinda dhidi ya vitendo hivyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Foundation,Tully Mwambapa, anabainisha kuwa wanaendelea kuwawezesha wanawake wajasiriamali wadogo kwa kuwapatia elimu ya fedha, mikopo na msaada wa kukuza biashara zao.
Anasema, “Wanawake wa biashara ndogo wanapewa mikopo, ushauri wa kifedha, na msaada wa kuanzisha na kukuza biashara zao. Hii inawasaidia kupata mapato ya kudumu na kuimarisha familia zao” (Chanzo: CRDB Bank, 2025).

Naye Meneja Mafunzo na Usimamizi kutoka CRDB Foundation, Joshua Mwakalobo
akimwakilisha Mkurugenzi Mtendaji huyo, anasema wamekutana na wajasiriamali wadogo wa mboga mboga na kubaini kuwa ni kundi muhimu sana kwa jamii.
“Hawa ni watu muhimu kwa jamii, tunaimarika siku zote kupitia bidhaa bora wanazozalisha na kuuza,” anasema.
Anaongeza kuwa lengo lao ni kuwajengea uwezo kwa kuwapatia elimu ya fedha sambamba na mitaji kulingana na mahitaji ya biashara zao.
“Huwezi kumpatia mtu elimu ya fedha bila kumpatia mtaji. Tunakwenda kuwapatia mitaji kulingana na uhitaji wa biashara zao,” anafafanua.
Kupitia programu ya Embeju, taasisi hiyo inalenga kutoa mitaji isiyo na riba na isiyokuwa na masharti magumu ili kuwasaidia wajasiriamali wadogo kuinuka kiuchumi.
Taasisi mbalimbali zinazohusiana na biashara na jinsia, zikiwemo mashirika ya maendeleo ya wanawake na asasi za kiraia, zinasema,
“Uwepo wa sera rafiki kwa wanawake, mafunzo ya ujasiriamali, na mbinu za masoko ni muhimu kwa maendeleo endelevu ya wanawake wajasiriamali.
Wanawake wanapaswa kushirikishwa katika maamuzi ya kibiashara na kupewa nafasi ya kuendeleza biashara zao bila vikwazo vya kijinsia” (Chanzo: Taasisi za Biashara na Jinsia, 2025).

