Na Danson Kaijage
DODOMA: TAASISI ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), kwa kipindi cha miaka minne imeona wagonjwa 745,837 kati ya hao watu wazima walikuwa 674,653 na watoto 71,184.
Aidha wagonjwa waliolazwa walikuwa 30,645 kati ya hao, watu wazima wakiwa 25,273 na watoto 5,372.
Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Dkt. Peter Kisenge amesema hayo alipokuwa akielezea mafanikio ya hospitali hiyo ya uongozi wa serikali ya awamu ya nne.
Amesema wagonjwa waliotibiwa JKCI Upanga walikuwa 513,484 kati ya hao watu wazima 470,119 na watoto 43,365 wagonjwa waliolazwa walikuwa 17,668 watu wazima wakiwa 14,580 na watoto 3,088.
Ametaja huduma zinazotolewa na taasisi hiyo kuwa ni matibabu ya moyo, kinywa na meno, huduma za dharura, kliniki ya wanawake na wajawazito, kliniki ya watoto, macho, pua, masikio na koo, kliniki ya ngozi, vibofu vya mkojo, upasuaji mkubwa na mdogo, magonjwa ya tumbo na ini, figo na matibabu mengine ya magonjwa yanayoambukiza kama malaria.
Akizungumzia huduma za tiba mkoba zijulikanazo kwa jina la Dk. Samia Suluhu Hassan Outreach Services amesema zimetolewa katika mikoa 20 na maeneo ya kazi 14 kwa watu 21,324 watu wazima wakiwa 20,112 na watoto 1,212 walifanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo.
Amesema kuwa kati ya hao 8,873 watu wazima wakiwa 8,380 na watoto 493 walikutwa na matatizo mbalimbali ya moyo na kuanzishiwa matibabu.
“Wagonjwa 3,249 watu wazima 2,765 na watoto 484 walikutwa na matatizo yaliyohitaji matibabu ya kibingwa na kupewa rufaa ya kuja kutibiwa katika Taasisi yetu.
“Wataaamu wetu walivuka mipaka ya nchi na kwenda kutoa huduma za matibabu ya moyo katika nchi za Malawi, Zambia na Jamhuri ya Watu wa Comoro wakiwa katika nchi hizo walitibu wagonjwa 1,189 watu wazima walikuwa 851 na watoto 338. Wagonjwa 262 walipewa rufaa ya kuja kutibiwa JKCI,”amesema.
Pia amesema wagonjwa waliotibiwa kutoka nje ya nchi walikuwa 689.
“Wagonjwa hao walitoka katika nchi za Somalia, Malawi, Kenya, Rwanda, Jamhuri ya Watu wa Comoro , Msumbiji, Nigeria, Siera Leone, Zimbabwe, Zambia, Uganda, Congo, Ethiopia, Burundi na wengine kutoka nje ya Afrika zikiwemo nchi za Armenia, China, Ujerumani, India, Norway, Ufaransa na Uingereza.
“Wagonjwa waliofanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo wa kufungua kifua na kubadilishwa Valvu za moyo moja hadi tatu, upasuaji wa kupandikiza mishipa ya damu ya moyo, upasuaji wa mishipa ya damu na mapafu walikuwa 2,784 kati ya hao watu wazima walikuwa 1,880 na watoto 904.”amesema.
Kwa upande mwingine amesema, Sh. Bilioni 2.16 zilitolewa na Serikali kwa ajili ya ukarabati wa vyumba vya watoto mahututi na chumba cha wagonjwa mahututi cha watu wazima, ukarabati na utanuzi wa ICU ya watoto ambayo hapo awali ilikuwa na vitanda nane na hivi sasa ina vitanda 16 na ICU ya wakubwa ambayo imetanuliwa na kuwa na vitanda 10 kutoka nane.