Na Mwandishi Wetu
DAR ES SALAAM: MFUKO wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umetunukiwa tuzo ya mshindi wa kwanza ya umahiri katika uaandaji wa taarifa za mahesabu kwa mwaka unaoishia 2023, katika kundi la hifadhi ya jamii.
Meneja wa Fedha PSSSF, Vonness Koka alipokea tuzo hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu katika hafla ya utoaji tuzo ulioratibiwa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu Tanzania (NBAA), ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkaguzi Mkuu wa Ndani, Wizara ya Fedha, Benjamin Mashauri.

“Tunamshukuru Mungu kwa kupewa hii tuzo, tunapokea tuzo hii kwa mara ya tatu mfululizo, pongezi kwa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko, Mkurugenzi Mkuu na Menejimenti yake na watumishi wote wa PSSSF kwa ujumla.
“Hususani kurugenzi ya fedha kwa kuwezesha kupatikana kwa tuzo hii. Tuzo hii iwe chachu ya kuhakikisha kwamba mahesabu yetu yanaandaliwa vyema kila wakati,” amesema Vonness.