Na Mwandishi Wetu
NCHI wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) zimehimizwa kuimarisha umoja na ushirikiano ili kukabiliana na changamoto zinazoibuka duniani zinazoweza kuathiri usalama na uchumi wa ukanda huo.
Wito huo umetolewa Julai 16, 2026 mjini Salima, Malawi, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 28 wa Kamati ya Mawaziri wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama ya SADC.

Ujumbe wa Tanzania umeongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (EAC), James Millya, akifuatana na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Ayoub Mohammed Mahmoud.
Katika mkutano huo, Tanzania imesisitiza umuhimu wa kuwa na mkakati madhubuti wa kubaini mapema viashiria vya uvunjifu wa amani na vihatarishi vya uchumi ili kuimarisha amani na usalama katika nchi za SADC.

Mwenyekiti wa mkutano huo ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa Malawi, George Chaponda, amesema pamoja na mafanikio yaliyopatikana katika kuimarisha mtangamano wa kikanda na utawala bora, bado kuna umuhimu wa kuendeleza ushirikiano na majadiliano kwa manufaa ya wananchi wa SADC.
Mkutano huo ulioanza Julai 13, 2026 katika ngazi ya Makatibu Wakuu unajadili masuala ya amani, usalama, demokrasia, utawala bora na maendeleo endelevu kwa lengo la kuhakikisha Kanda ya SADC inaendelea kuwa tulivu na salama.


