Na Lucy Lyatuu
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Paschal Katambi Patrobass, ametembelea Banda la Jeshi la Zimamoto na Uokoaji katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, Dar es Salaam.
Katika ziara hiyo, Katambi amepata fursa ya kutembelea na kujionea vifaa na mitambo mbalimbali ya kisasa inayotumiwa na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji katika shughuli za kuzima moto, uokoaji na kukabiliana na majanga mbalimbali.

Vifaa hivyo ni sehemu ya maboresho makubwa yaliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita kwa lengo la kuimarisha uwezo wa Jeshi katika kulinda maisha na mali za wananchi.
Maofisa wa Jeshi walimpa Waziri maelezo kuhusu matumizi ya vifaa hivyo, uwezo wake wa kukabiliana na matukio mbalimbali ya dharura, pamoja na namna vinavyorahisisha utoaji wa huduma za haraka na zenye ufanisi kwa wananchi.
Akizungumza baada ya kutembelea banda hilo, Katambi amelipongeza Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kuendelea kuimarisha uwezo wake wa kitaalamu na matumizi ya teknolojia ya kisasa katika utekelezaji wa majukumu yake.

Aidha, ameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt Samia Suluhu kuendelea kuwekeza katika ununuzi wa vifaa vya kisasa vinavyoongeza uwezo wa Jeshi kukabiliana na majanga na kutoa huduma bora kwa wananchi.
Kwa upande wake, uongozi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji umemshukuru Waziri kwa kutembelea banda hilo na kuendelea kutoa ushirikiano na mwelekeo unaowezesha Jeshi kuendelea kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi.
Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linaendelea kutumia Maonesho ya Sabasaba kutoa elimu kwa umma kuhusu kinga dhidi ya majanga ya moto, tahadhari za usalama, huduma za uokoaji, pamoja na kuhamasisha wananchi kupiga namba ya dharura 114 wanapokumbana na matukio ya moto au dharura nyingine zinazohitaji huduma za Jeshi.


