Na Mwandishi Wetu
BALOZI wa Tanzania nchini Ujerumani, Hassan Mwamweta, ameongoza ujumbe wa wakulima na wafanyabiashara kutoka Tanzania kushiriki Maonesho ya Kimataifa ya Matunda na Mboga mboga ya ‘Fruit Logistica 2026’ yaliyofanyika jijini Berlin kuanzia Februari 3 hadi 6, mwaka huu 2026.
Ujumbe huo unajumuisha Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka, pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), Saleh Saad Mohamed.

Taarifa inaeleza lengo la ushiriki wao ni kutafuta na kupanua masoko ya mazao ya Tanzania hususan parachichi, kuongeza mtandao wa wafanyabiashara, pamoja na kujifunza fursa na mbinu mpya katika kilimo-biashara.
Zaidi ya kampuni 40 kutoka Tanzania, kwa kushirikiana na Chama cha Wakulima wa Mazao ya Bustani Tanzania (TAHA), Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA) pamoja na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB), zinashiriki maonesho hayo.
Kwa ujumla, maonesho ya Fruit Logistica 2026 yamewakutanisha zaidi ya kampuni 2,600 kutoka nchi 151 duniani.

Fruit Logistica ni maonesho makubwa ya kimataifa yanayowaleta pamoja wakulima, wasambazaji, wanunuzi, wasafirishaji na wadau mbalimbali katika mnyororo wa thamani wa matunda na mbogamboga kutoka sehemu mbalimbali duniani.

