Na Lucy Ngowi
Mbunge wa Misenyi, Florent Kyombo, ameuliza katika kipindi cha maswali na majibu bungeni mjini Dodoma, “Je, lini Uwanja wa Ndege wa Kyabajwa utaanza kujengwa?”
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Uchukuzi,David Kihenzile amesema kuwa Serikali imekwishaanza utekelezaji wa mradi wa kiwanja kipya cha ndege katika Mkoa wa Kagera kwa kuingia mkataba na Mtaalamu Elekezi.
Mtaalamu huyo atafanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa kiwanja hicho kinachotarajiwa kujengwa katika eneo la Kyabajwa.
Naibu Waziri alifafanua zaidi kuwa Mtaalamu Elekezi anatarajiwa kukabidhiwa eneo la kazi na kuanza kazi ndani ya robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2025/2026.
Aidha, kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina imepangwa kukamilika mwishoni mwa mwaka 2026, na baada ya hapo hatua za utekelezaji wa mradi huo zitaanza rasmi.

