Na Lucy Ngowi
DODOMA: MBUNGE wa Jimbo la Ilongelo, Hidary Gulamali, ameibua hoja Bungeni akiitaka Serikali kueleza mpango wake wa kuboresha huduma za mawasiliano kwa kujenga minara ya simu katika maeneo yenye changamoto ya mtandao na mawasiliano ya simu ndani ya jimbo lake.
Gulamali ametoa hoja hiyo wakati wa kipindi cha maswali na majibu katika kikao cha Bunge kilichofanyika jijini Dodoma, akieleza kuwa ukosefu wa mawasiliano ya uhakika umekuwa kikwazo kikubwa kwa wananchi, hasa katika nyanja za kiuchumi, elimu na shughuli za kijamii.
Amezitaja kata za Namuhunga na Ilongelo kuwa miongoni mwa maeneo yaliyoathirika zaidi, ambapo wananchi hulazimika kutembea umbali mrefu ili kupata huduma za simu na intaneti.
“Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga minara ya mawasiliano katika kata za Namuhunga na Ilongelo zilizopo Jimbo la Singida Vijijini?” alihoji mbunge huyo.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Switbert Mkama, amesema Serikali imeshatambua changamoto ya mawasiliano inayokabili maeneo mbalimbali nchini, hususan vijijini, na tayari imeanza kuchukua hatua za makusudi kuikabili.
Amefafanua kuwa Serikali imeandaa mkakati wa miaka mitano unaolenga kujenga minara ya mawasiliano katika maeneo yote yenye upungufu wa huduma hiyo, kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata mawasiliano ya uhakika na yenye ubora.
Dkt. Mkama amemhakikishia mbunge huyo kuwa kata za Namuhunga na Ilongelo pamoja na maeneo mengine yenye changamoto katika Jimbo la Singida Vijijini zitahudumiwa kupitia utekelezaji wa mkakati huo pindi utakapotekelezwa kikamilifu.

