Na Lucy Ngowi
DODOMA: WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe, amesema kuwa Sh.Milioni 96 zimetengwa kwa ajili ya ukarabati wa Shule ya Msingi Mkwajuni mkoani Lindi, iliyoharibiwa na mvua na upepo.
Profesa Shemdoe ameeleza hayo wakati akijibu swali la nyongeza lililoulizwa na Mbunge wa Nchinga, Salma Kikwete (CCM), aliyeeleza kuwa katika Shule ya Mkwajuni madarasa mawili yaliezuliwa na upepo, hali iliyosababisha wanafunzi kushindwa kuendelea na masomo darasani.
Aidha, nyumba mbili za walimu pamoja na ofisi ya mkuu wa shule nazo ziliharibiwa.
Akijibu swali hilo, Profesa Shemdoe amesema tayari amemwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi kufika katika shule hiyo na hatua za awali zimechukuliwa.
“Tayari nimemwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi kwenda katika Shule ya Mkwajuni, na ameshakwenda. Kiasi cha Sh. Milioni 96 kimeshapelekwa kwa ajili ya kurekebisha madarasa yaliyoathirika.
“Serikali tayari imelichukua jambo hili, na nimshukuru Naibu Waziri wa Elimu kwa namna alivyolielezea,” amesema Profesa Shemdoe.
Waziri huyo pia ametoa pole kwa wananchi wa Nchinga, hususan wakazi wa Kijiji cha Mkwajuni, kutokana na tukio hilo.
Awali, Mbunge wa Nchinga, Salma Kikwete, alitoa pole kwa wananchi wa eneo lake kutokana na kadhia iliyotokea Januari 29, 2026, katika Shule ya Mkwajuni.
Amehoji kauli ya Serikali pamoja na mkakati wa haraka wa kuhakikisha wanafunzi wanarejea shuleni na kuendelea na masomo yao.

