Na Lucy Ngowi
MWENYEKITI wa Bunge Sports Club, Festo Sanga, ametangaza kufanyika kwa Bunge Bonanza 2026 kubwa litakalowakutanisha mashabiki wa timu kongwe za Simba na Yanga, lililoandaliwa na Benki ya Azania.
Bonanza hilo linatarajiwa kufanyika Januari 31, 2026 katika viwanja vya Shule ya Sekondari ya John Merlin, jijini Dodoma.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Ukumbi wa Bunge Msekwa, Sanga alisema bonanza hilo linalenga kuhamasisha michezo, afya na mshikamano, huku mashabiki wa Simba na Yanga wakikutana kwa amani, furaha na burudani.

Alisema mashabiki wa michezo wanakaribishwa kushiriki na kushuhudia jumla ya michezo 21 itakayochezwa siku hiyo, ikiwemo mchezo wa mpira wa miguu kati ya Simba na Yanga pamoja na michezo mingine ya burudani na afya.
Sanga aliongeza kuwa mgeni rasmi katika Bunge Bonanza 2026 atakuwa Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba.
Alisema kutakuwa na maandamano ya amani yatakayoanza saa 12 asubuhi, yakielekea katika viwanja vya John Merlin ambako bonanza hilo litafanyika.
Aidha, Benki ya Azania imethibitishwa kuwa mdhamini mkuu wa bonanza hilo kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo.
Akizungumza kuhusu ushiriki wa benki hiyo, Meneja Mahusiano wa Benki ya Azania, Elizabeth Nyatega, alisema michezo ina mchango mkubwa katika kukuza afya ya jamii.

“Benki ya Azania itaendelea kushirikiana na Serikali, Bunge na wadau wa michezo katika kukuza sekta ya michezo, vipaji na afya za Watanzania,” alisema Nyatega.
Aliongeza kuwa siku ya bonanza, benki hiyo itatoa huduma zote za kibenki kwa ajili ya kuwahudumia washiriki na wageni watakaohudhuria.
Katika hatua nyingine, Nyatega alikabidhi vifaa mbalimbali vya michezo kama sehemu ya maandalizi ya kuelekea Bunge Bonanza 2026.

