Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: CHAMA cha Wanahabari Wanawake Tanzania (TAMWA) kimetoa pongezi kwa wanawake wote waliojitokeza kugombea nafasi za uongozi kuanzia ngazi ya udiwani, ubunge hadi urais, katika kuelekea Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, mwaka huu 2025.
Mkurugenzi Mtendaji wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben ametoa pongezi hizo katika taarifa aliyoitoa kwa vyombo vya habari.
Amesema takwimu za Ulingo wa Wanawake zinaonesha jumla ya wanawake 231 walichukua fomu za ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambapo 25 kati yao waliteuliwa kuwa wagombea rasmi, wakiwemo wanawake wapya tisa jambo linaloashiria ari na mwamko mkubwa wa wanawake kushiriki katika siasa.
Amesema TAMWA imeonyesha furaha yake kwa kuteuliwa kwa Samia Suluhu Hassan kuwa mgombea urais kwa mara ya pili kupitia CCM, akiwakilisha mwanamke wa kwanza kuwa mgombea urais wa chama tawala katika historia ya Tanzania.
“Hatua hiyo inaelezwa kuwa ni mwelekeo mpya na chachu kwa ushiriki wa wanawake katika nafasi za juu za uongozi wa kitaifa,” amesema.
Pia amesema chama hicho kimewatambua na kuwapongeza wanawake wengine walioteuliwa kugombea urais kupitia vyama mbalimbali vya siasa, akiwemo Mwajuma Mirambo (UMD) aliyemchagua Mashavu Haji kuwa mgombea mwenza wake.
Wagombea wenza wanawake wengine ni pamoja na Eveline Munis (NCCR), Husna Abdallah (CUF), Aziza Selemani (MAKINI), Amani Mzee (TLP), Chausiku Mohamed (NLD), Sakia Debwa (SAU), Chuma Abdallah na Devotha Minja (CHAUMA).
Amesema hatua hiyo ni matokeo ya juhudi za muda mrefu za kuwawezesha wanawake kupitia warsha, makongamano, mijadala, na vipindi vya redio na runinga vyote vikiwa na lengo la kuondoa vikwazo vinavyowakabili wanawake katika siasa na uongozi.
Ripoti ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ya Februari 2024 inaonesha kuwa wanawake walikuwa asilimia 37.4 ya wabunge (148 kati ya 392), wengi wao kupitia viti maalum.
Aidha, ripoti za Aprili na Julai 2024 zinaonesha kuwa asilimia 37.5 ya mawaziri ni wanawake ishara ya maendeleo ya usawa wa kijinsia katika Serikali.
Kwa maelezo yake TAMWA bado kuna changamoto zinazoikabili jamii, hasa kutokana na mfumo dume na udhalilishaji wa wanawake katika mitandao ya kijamii.
Kwa sababu hiyo, chama hicho kitaendelea kutoa elimu kupitia vyombo vya habari kuhakikisha wanawake wanasiasa wanashiriki kampeni katika mazingira salama na yenye usawa kama ilivyo kwa wanaume, bila ubaguzi wa kijinsia.
“Uwepo wa wanawake kwenye uongozi ni muhimu kwa maendeleo ya taifa. Unaleta uwakilishi wa makundi yote, uwajibikaji na kulinda maslahi ya wanawake na watoto,” amesema.
Aidha, TAMWA imesisitiza wajibu wa jamii, vyama vya siasa, Serikali na wadau wa maendeleo kuhakikisha wanawake wanapata nafasi sawa katika siasa na uongozi ili kujenga taifa lenye usawa wa kijinsia, amani na maendeleo endelevu.
Chama hicho pia kimetoa wito wa kampeni safi na jumuishi, zenye staha na heshima kwa utu wa jamii, kikiwataka wanasiasa kuachana na siasa za matusi na kejeli.
“TAMWA itafuatilia kampeni zote na haitasita kuripoti mgombea au kundi lolote litakalokiuka kanuni za uchaguzi kwa mujibu wa sheria,” amesema.