Na Mwandishi Wetu
DODOMA: WANAFUNZI na Watumishi kutoka Shule ya Awali na Msingi ya Aswwiddiq iliyopo Temeke Jijini Dar es Salaam wametembela Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) kwa ajili ya kujifunza Teknolojia bora za Kilimo ili kujiongezea ujuzi na ari ya kukipenda Kilimo.
Wanafunzi hao 431 na Watumishi 52 wametembela TARI Juni nne , mwaka huu 2025 katika kituo chake cha Uhaulishaji wa Teknolojia za Kilimo kilichopo Nzughuni Nanenane Jijini Dodoma.
Akieleza kuhusu ziara hiyo, Mwanafunzi Hafidh Kagi amesema elimu aliyopata inamsaidia kuona umuhimu wa kufanya kilimo chenye tija ambacho kinafuata kanuni bora kuanzia utambuzi wa afya ya udongo, kupanda kwa nafasi na kuhudumia mazao.

Naye Mwanafunzi Najat Mambi, ameeleza kunufaika kwa kupata elimu ya kanuni bora za Kilimo pamoja na kuona mazao ambayo amekuwa akisoma.
Kwa upande wake Mwalimu Mkuu wa Shule, Mumo Athumani ameipongeza TARI kwa kazi wanazofanya ya kungundua Teknolojia bora za kilimo zenye kuongeza tija kwa Wakulima na Pato la Taifa kwa ujumla.
“TARI inafanya KAZI nzuri na kubwa ya kugundua teknolojia, hii inaongeza pato la mtu Mmoja na taifa kwa ujumla na sisi kama Shule elimu tuliyopata tunaenda kuanza walau kwa kuanzisha bustani shuleni itakayokuwa inahudumiwa na wanafunzi na Watumishi ili kujifunza Kilimo kwa vitendo,” amesema.

Kwa upande wa TARI, Mtafiti Mwandamizi Mshaghuley Ishika amepongeza uongozi na wanafunzi wa Shule ya Aswwiddiq kutembelea TARI kwa lengo la kujifunza Kilimo huku akitoa wito kwa shule zingine kuiga mfano huo wa kuwajengea mazingira wanafunzi kujifunza na kukipenda Kilimo.
Aidha Ishika alisema ujio wa wanafunzi na watumishi hao ni moja ya njia za TARI kuwafikia wadau mbalimbali wa kilimo kupata Teknolojia zinazobuniwa.