Na Mwandishi Wetu
Dar es Salaam: KAMISHNA wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Amina Talib Ali, amesema Tume hiyo ni mdau mkubwa katika utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Mwandishi Mkuu wa Sheria (OCPD) hasa katika kuhakikisha zinaandikwa kwa kuzingatia haki na utawala bora.
Amesema hayo alipotembelea Banda la OCPD kwenye maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara yajulikanayo kama SabaSaba yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwalimu Nyerere Jijini Dar es salaam.
“Moja ya vitu vya msingi THBUB inatakiwa kuzingatia ni kuhakikisha kuwa sheria zinazotungwa zinazingatia mikataba ambayo Tanzania imeridhia kuhusiana na haki za binadamu na utawala bora.
“Kwa minajili hiyo, sisi ni wadau wakubwa wa mchakato mzima wa uandishi wa sheria.” amesema.
Katika kufafanua ushiriki wa THBUB katika mchakato mzima wa uandishi wa sheria, ameeleza kwa mujibu wa Ibara ya 130 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano na kifungu cha sita cha Sheria ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Sura ya 391,
“THBUB ina majukumu ya kutoa mapendekezo kuhusu sheria zilizopo au zinazopendekezwa, kanuni au masharti ya kiutawala kwa madhumuni ya kuhakikisha uzingatiaji wa misingi ya haki za binadamu na utawala bora.
Amesema pia THBUB inahamasisha kuridhiwa au kujiunga na mikataba au makubaliano yanayohusiana na haki za binadamu ikiwa ni Pamoja na kuratibu sheria za Tanzania ziendane na mikataba hiyo, kufuatilia na kutathmini uzingatiaji wa haki za binadamu ndani ya Jamhuri ya Muungano, Serikali au watu wengine.
Kamishna huyo amesema Tanzania ni moja kati ya nchi ambazo zimeridhia mikataba mingi ya kimataifa inayohusu haki za binadamu na utawala bora hivyo katika utekelezaji wa shughuli zake, lazima ihakikishe haivunji kipengele chochote katika mkataba iliyoiridhia katika nyanja hizo.
“Naielewa sana kazi nzuri na kubwa mnayoifanya katika uandishi wa sheria za nchi, na tunatambua mchango wenu katika kuhakikisha mapendekezo ya kutunga au kurekebisha sheria na sera zinazoletwa kwenu kwa ajili ya kuzifanya kuwa sheria.
“Hakika mnafanya kazi nzuri ya kuzingatia mambo muhimu ya haki za binadamu na utawala bora zinazingatiwa.” amesema.
Naye Mwandishi wa sheria kutoka OCPD, Philemon Mrosso amemueleza Kamishna majukumu makuu ya tume hiyo kuwa ni kuandika sheria, kufanya urekebu wa sheria, kufanya ufasili wa sheria pamja na nyaraka zote za kisheria zinazowasilishwa Bungeni na masuala mengine yote yanayohusiana na uandishi wa sheria.
Amesema ili kuwezesha utekelezaji wenye ufanisi wa majukumu ya Ofisi hiyo, wamekuwa wakitoa mafunzo ya mara kwa mara kwa waandishi wa sheria na mawakili wa serikali kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kufahamu masuala yote ya msingi wakati wa uandishi wa sheria.
Akieleza kuhusu kusitishwa kutumika kwa Toleo la Urekebu wa Sheria la Mwaka 2002 pamoja na matoleo mengine yote yaliyofuata, Mwandishi wa Sheria kutoka tume hiyo Vincent Masalu amewataka wadau wa sheria nchini kutambua kuwa toleo hilo limesitishwa kutumika rasmi Julai Mosi, 2025 kufuatia tamko rasmi la Rais alilolitoa Aprili 24, mwaka huu 2025 wakati akizindua Toleo la Urekebu wa Sheria la Mwaka 2023.
“Toleo jipya la urekebu la mwaka 2023 lenye jumla ya sheria kuu 446 zilizofanyiwa Urekebu ndilo limeanza kutumika kuanzia Julai mosi, 2023, hivyo kuanza kutumika kwa Toleo jipya la mwaka 2023 kunasitisha matumizi ya matoleo yote ya urekebu ya miaka ya nyuma kabla ya toleo hili jipya la urekebu la mwaka 2023” amesema Masalu.
Masalu alieleza kuwa kwa kutekeleza amri hiyo ya Rais, Sheria zote zilizofanyiwa urekebu mwaka 2023 tayari zimewekwa katika tovuti ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, nakala mango za sheria hizo zinaendelea kusambazwa katika Wizara na taasisi zote za umma, lakini pia nakala nyingine za sheria hizi zinasambazwa na kuuzwa kwa wananchi wote.
Katika hatua nyingine Mwandishi wa Sheria Mariam Possi, amewasihi wananchi, wadau na umma kwa ujumla kufika katika banda la OCPD ili kuweza kupata elimu kuhusiana na mchakato mzima wa uandishi wa sheria nchini na kupata fursa ya kuona majuzuu ya Toleo la Urekebu wa Sheria la Mwaka 2023 pamoja na kupata nakala ya machapisho mbalimbali yanayotumika na Ofisi yetu katika kutekeleza majukumu yake