Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya TotalEnergies Marketing Ltd kwa kushirikiana na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), wamekabidhi madawati 130 katika Shule ya Msingi Jaribuni Mpakani na Shule ya Msingi ya Kitunduza Wilayani Kibiti mkoa wa Pwani ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ushirikiano baina yao Katika kuboresha miundombinu ya elimu nchini.
Mkuu wa Wilaya ya Kibiti Kanali Joseph Kolombo aliongoza hafla ya kukabidhi madawati hayo iliyofanyika Shule ya Msingi Jaribuni Mpakani.
Kolombo Katika hafla hiyo aliagiza madawati hayo yatunzwe vizuri kwa manufaa ya wanafunzi wa shule hiyo, na kuongeza kuwa wamekuwa wakinufaika na miradi mbalimbali ya TEA ikiwemo wa ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum Katika Shule ya Msingi Kitundu.
Naye Mkurugenzi wa Sheria na Mahusiano wa TotalEnergies Marketingi Tanzania Ltd, Getrude Mpangile amesema madawati hayo 130 ni sehemu ya madawati 200 yenye thamani ya sh milioni 25.9 yaliyotolewa na kampuni hiyo kwa shule tatu za Mkoa wa Pwani na Dar es Salaam.
Kutokana na msaada huo Shule ya Msingi Jaribuni Mpakani imepata madawati 65, Shule ya Msingi Kitundu madawati 65 na Shule ya Msingi Makukburi ya Mkoani Dar es Salaam madawati 70.
Ameelezea matumaini yake kuwa msaada huo utasaidia kuweka hamasa kwa wanafunzi kujifunza kwa bidii hivyo kuchangia kukuza ufanisi na ufaulu wa shule zilizonufaika na madawati hayo.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Taasisi TEA, Mwanahamisi Chambega amekumbusha shule zilizonufaika na msaada huo wa madawati kuyatunza vyema.
“Miongoni mwa majukumu ya TEA ni kutafuta rasilimali fedha kutoka kwa wadau mbalimbali na kuzigawa Katika Taasisi za Elimu ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia hivyo tunawakumbusha kutunza vifaa hivi,” amesema.