Na Lucy Lyatuu,Dodoma
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano ya Kazi), imesema miongoni mwa sababu zinazotajwa kuchangia ukosefu wa ajira kwa vijana ni kutokuwa na ujuzi sahihi unaowawezesha kujiajiri au kuajiriwa katika sekta mbalimbali za kiuchumi.
Aidha imesema itaendelea kuratibu na kuboresha sera, sheria na miongozo ya programu ya mafunzo ya uanagenzi, pamoja na kuhamasisha sekta binafsi kushiriki kikamilifu katika kutoa nafasi za mafunzo kwa vitendo kwa vijana.
Waziri wa Wizara hiyo Deus Sangu amesema hayo na kuwataka wanagenzi kuonesha nidhamu, bidii, ubunifu, uaminifu na uadilifu wawapo vyuoni na katika maeneo ya mafunzo kwa vitendo.
Amesema hayo katika hafla ya uzinduzi wa mafunzo ya Uanagenzi awamu ya nane ya stadi za kazi kwa njia ya uanagenzi kwa mwaka 2025/2026 kwa vijana 5,746 yanayoendelea katika vyuo 46 nchini alisema serikali itasimamia viwango vya ubora wa mafunzo hayo na kuweka mazingira rafiki ya ajira na uwezeshaji ili kuongeza fursa za ajira kwa vijana kupitia shughuli za serikali katika halmashauri na taasisi mbalimbali.
Ameongeza kuwa maendeleo ya nguvu kazi ya vijana ni sehemu ya Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2025–2030 ya Chama Cha Mapinduzi pamoja na utekelezaji wa Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa miaka mitano.
Aliwapongeza Chuo cha Ufundi cha Don Bosco kwa utekelezaji mzuri wa programu hiyo. Kwa muda mfupi vijana wamepata mafunzo yenye tija.
” Serikali ipo pamoja nanyi katika kuhakikisha mafanikio ya mpango huu. Natambua kuwa wanagenzi 480 wamepata udahili wa asilimia 100 kutoka serikalini,” amesema.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Zuhura Yunus, amesema lengo la uzinduzi huo ni kuitangaza programu ya kukuza ujuzi na kuhamasisha vijana wengi zaidi kushiriki bila kukosa fursa hizo.
Amesema pia hatua hiyo inalenga kuimarisha ushirikiano kati ya serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo, pamoja na kusisitiza umuhimu wa ujuzi katika kukuza ajira na uchumi wa taifa.

