Na Danson Kaijage
DODOMA: MKUU wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyamule amewaagiza wakuu wa wilaya zote za mkoa huo kufanya tafiti na kurejesha majibu haraka juu ya hali ya chakula katika maeneo yao.
Senyamule ametoa maagizo hayo kwenye kikao cha kamati ya Ushari Mkoa wa Dodoma kilichokuwa kikijadili mambo mbalimbali ya kimaendeleo ikiwemo hali ya ukame inayoendelea nchini.
Kiongozi huyo wa Mkoa amesema kuna kila sababu ya kufanya utafiti wa kina ili kujua hali ya chakula ikoje kila wilaya kwa nia kuweka utaratibu wa kujipanga kukabiliana na hali hiyo pindi itakapoonekana kuna hali ya uhitaji wa chakula hapo mbeleni.
Katika hali nyingine amewataka wananchi wa Mkoa wa Dodoma kuhakikisha wanatunza chakula, wasitumie nafaka kwa ajili ya kutengenezea pombe
Kutokana na hali ya ukame inayoendelea amewashauri wafugaji kuvuna mifugo na kununua chakula huku akieleza kuwa kuna uwezekano mkubwa wa hata hiyo mifugo kukosa malisho kama hali ya hewa itaendelea hivyo.
Sambamba na hilo amehimiza juhudi za makusudi kuendelea kufanyika kwa kuwahimiza wakulima kulima kilimo cha umwagiliaji pale inapowezekana ili kufanikisha kupata mazao yanayostahili kulimwa sehemu husika.
Kwa upande mwingine, Mbunge wa jimbo la Kongwa Job Ndugai ametoa ushauri kwa Jiji kuona namna ya kufanya uwekezaji mkubwa ambao utabeba Mkoa mzima hasa kwa upande wa elimu.
Amesema kutokana na Jiji kuwa na mapato makubwa kuna kila sababu ya kujenga shule kubwa ya bweni ambayo itaweza kuwahudumia wanafunzi wengi ambao watakuwa wamekosa nafasi katika shule za wilaya wanazoishi.