Na Mwandishi Wetu
CHAMA cha Walimu Tanzania (CWT) kinawatakia waumini wote kipindi chenye baraka cha Kwaresma na Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Salamu hizo zimetolewa na Rais wa CWT, Dkt. Suleiman Ikomba, akieleza kuwa vipindi hivi adhimu katika kalenda za imani vinakumbusha umuhimu wa toba, subira, unyenyekevu, kujitafakari na kuimarisha upendo kwa jirani.
Amesema ni wakati wa kuongeza mshikamano, kusaidiana na kuendeleza maadili mema katika familia, maeneo ya kazi na jamii kwa ujumla.
Akizungumza na walimu, Dkt. Ikomba amesema kuwa wao ni nguzo muhimu ya malezi na makuzi ya Taifa, hivyo vipindi hivi viwe chachu ya kuimarisha wito wa ualimu kwa moyo wa kujitolea, uvumilivu na uzalendo.
Amewahimiza waendelee kuwa taa inayoangaza kizazi cha sasa na kijacho kwa maarifa na maadili.
Aidha, amewataka viongozi na wadau wa elimu kutumia kipindi hiki kuimarisha ushirikiano, maelewano na mshikamano katika kuendeleza sekta ya elimu kwa ustawi wa wanachama na Taifa kwa ujumla.
Amesisitiza umuhimu wa kudumisha amani, umoja na mshikamano kama msingi wa kufikia maendeleo endelevu ya CWT na nchi.
Amemwomba Mwenyezi Mungu awajalie wote afya njema, hekima na mafanikio katika kipindi hiki na baada yake.

