Na Mwandishi Wetu
MKUU wa Mkoa wa Njombe, Anthony Mtaka, amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Joseph Ndunguru, kuhusu utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa maabara ya kimkakati mkoani humo.
Mazungumzo hayo yalilenga kukabidhi rasmi mkandarasi atakayehusika na usanifu wa michoro pamoja na usimamizi wa ujenzi wa Maabara ya Kimkakati na jengo la utawala, miradi itakayojengwa katika Mji wa Serikali wa Lunyanywi.
Akizungumza katika kikao hicho, Profesa Ndunguru alisema TPHPA pia imepiga hatua katika kupanua masoko ya mazao nje ya nchi baada ya kusaini mkataba wa kupeleka bidhaa 60 nchini Malawi, zikiwemo aina 30 za mazao yatakayouzwa katika soko hilo.

Kwa upande wake, Mtaka alimshukuru Profesa Ndunguru kwa kutambua nafasi ya Njombe katika uzalishaji wa chakula nchini.
Alisema ujenzi wa maabara hiyo ya kimkakati utakuwa na mchango mkubwa kwa wakulima na wafanyabiashara wa mazao kwa kuwawezesha kupata huduma za kisayansi, uhakiki wa ubora na ushauri wa kitaalamu kwa wakati.
Aliongeza kuwa uwepo wa maabara hiyo utaimarisha zaidi biashara ya mazao ya kilimo kutoka Njombe kwenda masoko ya ndani na nje ya nchi, sambamba na kuongeza thamani ya mazao yanayozalishwa na wakulima wa mkoa huo.


