Na Danson Kaijage
DODOMA: WIZARA ya Elimu Sayansi na Teknolojia imefanya mapinduzi makubwa katika sekta ya elimu katika kipindi cha miaka minne ya Rais Samia Suluhu Hassan.
Kwamba katika kipindi hicho imeongeza bajeti kubwa kwa ajili uwezeshaji wa elimu ya Juu.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amesema hayo alipozungumza na Waandishi wa habari katika Ukumbi wa Idara ya Habari – MAELEZO kuelezea mafanikio ya miaka minne ya serikali ya awamu ya sita.
Amesema, “Ili taifa lolote liweze kuwa na maendeleo ni lazima lijengwe kwa misingi ya Elimu ambayo ina Sayansi na Teknologia ikiwa ni pamoja na ujuzi mbalimbali katika kuelewa mambo na kuzalisha kwa lengo la kuongeza uchumi wa nchi na uchumi wa mtu mmoja mmoja”.
Pia amesema kwa sasa mwanafunzi wa kitanzania atalazimika kusoma elimu ya lazima kwa miaka 10 ambapo akijiunga na kidato cha kwanza ataweza kujiunga na masomo ya Amali na Elimu ya Jumla.
amesema mwanafunzi atakayejiunga na masomo ya amali atajifunza masomo ya Ufundi na ufundi stadi pamoja na masomo mengine huku atakayejiunga na masomo ya jumla atajifunza masomo ya vitendo na masomo ya kawaida.
Vile vile amesema serikali imeanzisha somo la lazima ambalo kila mwanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne ni lazima ajifunze masomo ya ujasiliamali ikiwa ni pamoja na kuelewa umuhimu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania na namna ya umuhimu wa kusajili kampuni au biashara mbalimbali.
Kuhusu lugha amesema kwa sasa kuanzia darasa la kwanza wanafunzi wataweza kufundishwa lugha ya kiingereza bila kujali sheria za lugha hiyo ili kumjengea mtoto uwezo wa kujieleza.
Akizungumzia mikopo kwa Elimu ya Juu, amesema Wizara inatambua kuwepo kwa changamoto za utoaji mikopo na hiyo inatokana na ujazaji wa taarifa za mikopo lakini na kuona ni nani anastahili kupata mkopo bila upendeleo.