– Umegusa Changamoto, Vikwazo Vinavyowakabili Bodaboda
Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: MATOKEO ya Utafiti uliofanywa kuhusu Bodaboda wa Dar es Salaam, kuelekea Usafiri Endelevu na Uhakika wa Ustawi wa Maisha, utatambua mchango wa kiuchumi wa waendesha pikipiki wanawake hususan kwenye miji mikubwa.
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Felister Mdemu amesema hayo wakati wa uzinduzi wa taarifa ya utafiti kuhusu waendesha Pikipiki Wanawake Mkoani Dar es Salaam.
Mdemu amesema utafiti huo pia utasaidia kutambua changamoto na vikwazo vinavyowakabili katika kujikwamua kiuchumi.

Pia kutambua mahitaji ya wanawake waendesha pikipiki na mikakati ya kuongeza ushirika mpana wa kundi hilo.
Amesema lengo la serikali ni kuhakikisha inawawekea mazingira wezeshi na rafiki ili wafanyabiashara ndogo ndogo waweze kunufaika na fursa za kiuchumi na kijamii ikiwemo mikopo ya biashara kupitia Taasisi za fedha.
Amesema katika kukabiliana na changamoto zinazokwamisha maendeleo ya wafanyabiashara ndogo ndogo nchini, Wizara ya Maendeleo ya Jamii imeendelea na kazi ya kuratibu na kusimamia shughuli zao.
“Wafanyabiashara hao ni pamoja na wachuuzi wa bidhaa yaani machinga, mama/ baba lishe, waendesha bodaboda na bajaji, wasusi na wengine wote wenye mauzo ghafi yasiyozidi Sh. Milioni nne kwa mwaka.
“Utaratibu huu ubafanyika kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Wizara za kisekta pamoja na wadau.
“Hivyo matokeo ya utafiti huu ni ushahidi kuwa, serikali imedhamiria kushughulikia changamoto zinazolabili kundi hilo,” amesema.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Mawasiliano na Uchukuzi Tanzania (COTWU – T), Juliana Mpanduji amesema kuwa ukuaji wa Sekta isiyo Rasmi ni muhimu kwani unalenga maisha ya mtanzania katika uzalishaji na kuongeza kipato.
Amesema utafiti huo umelenga hasa kuboresha mazingira ya uzalishaji ambao umekuwa ukikua kwa kasi.
” Kushirikiana na Friedrich Ebert Stiftung (FES) kwa mchango wao muhimu na kukubali kufanya kazi na sisi bega kwa began ni jambo kubwa nakupongeza sana.
” Hii inaonyesha upendo wa dhati kwa Tanzania, wanawake na wasafirishaji kwa ujumla.
” Hasa zaidi imegusa moyo wangu kama mwanamke ninayeongoza chama chenye wafanyakazi wanaume wengi,” amesema.
Amesema kwa sasa hiyo ni ajira kwa vijana na wanawake wengi wanaojikwamua kiuchumi.
Amesema tafiti hiyo iliyozinduliwa imeangazia mambo mengi ya maisha ya kila siku ya madereva kuhusu kipato chao, na changamoto za kazi hiyo kwa kuwa mara nyingi haichukuliwi kama ni kazi yenye staha.
