Na Danson Kaijage
MTAALAM wa Uchumi, Masumbuko Mwaluko amechukua fomu kuomba ridhaa ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kumteua kugombea ubunge katika Jimbo la Manyoni ambalo awali lilikuwa likifahamika kama Manyoni Mashariki.
Akizungumza na waandishi wa habari leo mara baada ya kukabidhiwa fomu hiyo, amesema nia yake ni kuomba kuteuliwa na chama kuwa mgombea ubunge katika jimbo hilo ili kuisadia serikali kutatua changamoto mbalimbali za waanchi.

Amesema changamoto hizo ni pamoja na upatikanaji wa huduuma mbalimbali za kijamii ikiwamo maji, afya, elimu pamoja na miundombinu ili kuchochea maendeleo katika eneo hilo.
“Lakini pia nimshukuru Mwenyekiti wetu wa Chama ambaye pia ni Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan na msaidizi wake namba moja Katibu Mkuu CCM, Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi kwa kuweka kanuni na utaratibu mzuri wa uchukuaji fomu na urejeshaji,”amesema Mwaluko.
Naye Katibu wa CCM wilaya ya Manyoni, Maimuna Likunguni amesema hadi sasa katika majimbo mawili ya wilaya hiyo ikiwamo jimbo la Itigi jumla ya watiania 25 wamejitokeza kuchukua fomu kuomba ridhaa ya chama.
“Katika jimbo la Manyoni jumla ya watia nia tisa wamejitokeza kuchukua fomu na kati yao wawili ni wanawake lakini katika jimbo la Itigi wamejitokeza 16 na wawili kati yao ni wanawake.
“Uchukuaji fomu unaendelea vizuri na hakuna changamoto yoyote hadi sasa, nitumie fursa hii kuwaita wanachama wote wenye sifa kujitokeza kuitumia fursa hii iliyotolewa na chama chao ili kugombea,”amesema Likunguni