Na Lucy Ngowi
MBUNGE wa Jimbo la Bagamoyo (CCM), Subira Mgalu, ameuliza swali bungeni akitaka kufahamu iwapo Serikali ipo tayari kutenga fedha katika mwaka wa fedha 2026/2027 kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) katika wilaya hiyo.
Akiuliza swali hilo, Mbunge Mgalu amesema Halmashauri ya Bagamoyo tayari imetenga eneo na kulikabidhi kwa Mamlaka ya VETA kwa ajili ya ujenzi wa chuo hicho.
Ameongeza kuwa ujenzi wa chuo hicho pia umeainishwa katika Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

“Kwa kuwa Halmashauri ya Bagamoyo imetenga eneo na kulikabidhi VETA kwa ajili ya ujenzi wa chuo, na jambo hili lipo kwenye Ilani ya CCM,
“Je, Serikali ipo tayari kutenga fedha katika mwaka huu wa fedha 2026/2027 ili vijana wa Bagamoyo wapate stadi mbalimbali
zitakazowawezesha kushiriki katika miradi ya kimkakati inayotarajiwa kutekelezwa, ikiwemo ujenzi wa bandari?” alihoji Mbunge Mgalu.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wanu Ameir, amesema kuwa Serikali katika mwaka wa fedha 2024/2025 ilitenga Sh. Bilioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa awali wa vyuo vya VETA nchini.
Aliongeza kuwa kwa mwaka wa fedha 2025/2026, Serikali tayari imetenga Sh. Bilioni 21.262 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa awamu ya kwanza, pamoja na kuanza ujenzi wa vyuo vya VETA katika maeneo ambayo bado hayana vyuo hivyo.

