DAR ES SALAAM: KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi Taifa (NEC), Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Amos Makalla amewataka wagombea kutobweteka katika uchaguzi wa viongozi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa Novemba mwaka huu.
Makalla amesema hayo leo katika mkutano uliofanyika Wilaya ya Kinondoni Dar es Salaam.
“Pamoja na kwamba kuna dalili za wenzetu kutosimamisha wagombea maeneo mbalimbali, itakapotokea naomba nizungumze na wana CCM wa Kinondoni na nchi nzima, kwamba uchaguzi huu hauna kupita bila kupingwa msibweteke.
“Mmesikia chama Fulani kimesema tutahakikisha hata kama CCM ndio wameteuliwa, tutahakikisha kuhamasisha wananchi wanapowapigia kura za hapana.
“Na CCM tukasema wana CCM hatulali tuko imara, tutahakikisha pale ambako tuko peke yetu tutafanya kampeni za kuhakikisha wagombea wetu wanapata kura zote za ndio,”amesema.
Amesema wale wanaosubiri watasubiri kama mtu anayesubiri ndege bandarini badala ya kwenda uwanja wa ndege.
“Anayesubiri kumwangusha mgombea wa CCM kwa kura za hapana ni sawa na mtu anayesubiri ndege bandarini badala ya uwanja wa ndege, “amesema.