Na Mwandishi Wetu
Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imesisitiza kuwa utekelezaji wa mfumo wa ithibati kwa waandishi na watangazaji wa habari ni mkakati muhimu wa kukuza uaminifu, weledi na ushindani wa sekta ya habari katika uchumi wa kisasa unaotegemea taarifa sahihi na za kuaminika.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Patrick Kipangula, ameeleza hayo alipozungumza katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji (ABC) uliofanyika Februari 13, 2026 jijini Dodoma,
Alisema mfumo huo unalenga kuimarisha taaluma kwa kuzingatia misingi ya kitaaluma, maadili na uwajibikaji kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229.

Alifafanua kuwa ithibati si chombo cha kudhibiti maudhui ya habari, bali ni utaratibu wa kuweka viwango vinavyolinda hadhi ya taaluma na kuongeza imani ya umma kwa vyombo vya habari.
Aliongeza kuwa katika mazingira ya ushindani wa kidijitali, uaminifu wa chanzo cha habari ndiyo rasilimali kuu ya chombo cha habari.
Aidha, alieleza kuwa vyombo vinavyowekeza katika kuimarisha weledi wa watumishi wake hujiongezea nafasi ya kuvutia wawekezaji, matangazo na ushirikiano wa kimataifa, kutokana na kuongezeka kwa thamani ya ubora na uwajibikaji katika soko la habari.
Kwa mujibu wa wadau walioshiriki mkutano huo ulioandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ushirikiano kati ya msimamizi wa maudhui na wadau wa tasnia ni msingi muhimu wa kujenga sekta imara inayochangia maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Uimarishaji wa mfumo wa ithibati umeelezwa kuwa sehemu ya mkakati mpana wa Serikali wa kukuza taaluma za ubunifu na mawasiliano kwa viwango vinavyokidhi mahitaji ya ndani na kimataifa, huku sekta ya habari ikiendelea kuwa nguzo ya uwazi, uwajibikaji na maendeleo endelevu.
Takwimu zinaonesha kuwa zaidi ya waandishi 3,200 kati ya 3,900 walioomba vitambulisho vya uandishi wa habari (Press Card) wamekidhi vigezo vya kisheria na kuthibitishwa, jambo linaloashiria mwitikio chanya na dhamira ya sekta kujiimarisha kitaaluma.

