Na Lucy Lyatuu,Dodoma
TUME ya Ushindani (FCC), imesema katika kipindi cha robo mwaka imeatua malalamiko 63 yaliyowasilishwa ambapo malalamiko 45 yamepatiwa ufumbuzi huku malalamiko 19 yakiwa katika hatua mbalimbali za utatuzi.
KAIMU Mkurugenzi Mkuu wa FCC,Khadija Ngasongwa amesema hayo wakati akielezea mafanikio ya Tume hiyo na kuongea kuwa pamoja na kushughulikia malalamiko, Tume hiyo pia ina jukumu la kusajili mikataba mbalimbali kwa mujibu wa sheria.
Amesema mikataba hiyo hupitiwa ili kuhakikisha inazingatia taratibu na kulinda maslahi ya walaji pamoja na sekta ya kifedha.
Aidha, amebainisha kuwa taasisi za fedha hasa katika sekta ya mikopo ya kifedha haziruhusiwi kuongeza riba au kufanya mabadiliko katika programu zao bila kupitia Tume ya Ushindani kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa.

Pia ameongeza kuwa Tume ya Ushindani imekuwa ikifanya ushirikiano mkubwa na Benki Kuu ya Tanzania kwa kuwakutanisha wadau mbalimbali kujadili namna ya kuwalinda walaji hasa katika sekta za kifedha ambazo zimekuwa zikilalamikiwa na wananchi.
Amesema kuwa ushirikiano huo umefanyika kwa lengo la kuboresha huduma jumuishi za kifedha kupitia mifumo madhubuti ya kushughulikia malalamiko ya wateja ili kuhakikisha wanapata huduma bora.
Aidha amebainisha kuwa katika kuboresha huduma kwa wananchi, Tume imefanya ushirikiano na Wakala wa Vipimo pamoja na wadau wengine kufuatilia malalamiko ya watumiaji wa huduma za intaneti ambapo wananchi wengi wamekuwa wakilalamikia matumizi ya vifurushi vya data.
Amesema kuwa tafiti zinafanyika ili kuhakikisha wananchi wanapata thamani halisi ya fedha wanazolipia kulingana na huduma wanazotarajia.
Pia ameongeza kuwa hatua hizo zinalenga kusaidia kukuza uchumi wa nchi kwa kuhakikisha ushindani huru na wezeshi unaimarika pamoja na kuimarisha uchumi wa soko.
Aidha amebainisha kuwa katika utekelezaji wa dira ya maendeleo ya mwaka 2050, Tume inalenga kuhakikisha ushindani wa kibiashara unaimarika ili kuongeza nguvu ya ununuzi kwa wananchi na kuchochea mzunguko sahihi wa fedha katika uchumi.
Pia amebainisha kuwa Tume itaandaa vikao vya uelimishaji vitakavyowahusisha wazalishaji, walaji na Serikali kwa lengo la kujadili masuala muhimu yatakayosaidia kuboresha sekta hizo.
Amesema kuwa kupitia majadiliano hayo, Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara huku walaji wakipata huduma bora zaidi.
Aidha ameongeza kuwa Tume inaendelea kutekeleza miradi ya kidigitali kwa ajili ya kuboresha huduma zake kupitia mfumo wa Automation of Business Process.
Pia amebainisha kuwa katika kutekeleza mradi huo, Tume imeingia ubia na taasisi ya Trade Mark Africa ambapo kiasi cha dola za Marekani laki sita, sawa na takribani sh bilioni 1.4 kimetengwa kwa ajili ya kuboresha mifumo ya huduma pamoja na kuimarisha udhibiti wa bidhaa bandia nchini.

