Na Mwandishi Wetu
DODOMA: KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Maji na Mazingira imeidhinisha Randama ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Randama hiyo imejadiliwa na wajumbe wa kamati hiyo wakiongozwa na Mwenyekiti wake, Jackson Kiswaga, katika kikao kilichofanyika Bungeni jijini Dodoma.
Akiwasilisha randama hiyo kwa niaba ya Waziri wa Maji, Mkurugenzi Msaidizi wa Mipango na Bajeti wa Wizara hiyo, Tedy Mwaijumba, amesema kuwa randama hiyo imeainisha makadirio ya mapato na matumizi pamoja na vipaumbele vya wizara kwa mwaka ujao wa fedha.
Ametaja baadhi ya vipaumbele hivyo kuwa ni pamoja na kuendelea na utekelezaji wa miradi ya maji ya vijiji 867, ujenzi wa mabwawa 35, na miradi 220 ya maji mijini.
Vipaumbele vingine ni kuendeleza mradi wa kimkakati wa Mpango wa Mtandao wa Taifa wa Usambazaji Maji (Gridi ya Maji ya Taifa), kuimarisha usimamizi wa rasilimali za maji, pamoja na kuongeza uendelevu wa huduma za maji na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Aidha, wizara imepanga kupunguza upotevu wa maji, kuendeleza vyanzo mbadala vya fedha kwa ajili ya miradi ya maji, pamoja na kuimarisha taasisi zilizo chini ya wizara hiyo na mfumo wa uratibu wa utekelezaji wa miradi.
Kuidhinishwa kwa randama hiyo kunatoa fursa kwa Wizara ya Maji kuandaa hotuba ya bajeti ya mwaka 2026/2027 itakayowasilishwa katika Bunge la Bajeti.
Akizungumza baada ya kuidhinishwa kwa randama hiyo, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso ameishukuru kamati hiyo kwa ushirikiano wake na kuahidi kuwa wizara itazingatia maoni yaliyotolewa katika kuandaa hotuba ya bajeti.

