Na Lucy Ngowi
DODOMA: MPANGO wa kuweka vituo vya usindikaji wa zao la mkonge umewekwa kwa lengo la kumsaidia mkulima mdogi ili aweze kusindika na kupata nyuzi Singapore ambazo zitakubalika katika soko la ndani na nje ya nchi.
Mpango ambao umewekwa na Bodi ya Mkonge Tanzania (TSB), kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo.
Mkuu sehemu ya Maendeleo ya mkonge kutoka TSB,Simon Kibasa, amesema hayo katika maonesho ya wakulima, Wafugaji na Wavuvi yanayofanyika Kitaifa viwanja vya nane nane Nzuguni jijini Dodoma.
Kibasa amesema Bodi imekuwa ikiwaunganisha wakulima na masoko na kwamba sehemu ya masoko hayo ni kuwaunganisha wakulima hao ili wapate soko la bei nzuri.
Ameongeza kuwa nchini Tanzania wakulima wamegawanyika katika makundi matatu wadogo, wakubwa na wakati huku akisema wakulima wakubwa hawana changamoto kama ilivyo kwa wakulima hao wadogo.
“Na wakulima wadogo nao wamegawanyika katika sehemu mbili wanaolima kwenye mashamba yao binafisi na wanao fanyabiashara lakini wapo ambao wanalima kilimo cha mkataba kinachoendeshwa katika mashamba matano nchini yakiwamo Ngombezi na magoma,” amesema.
Amefafanua kuwa katika mashamba hayo yana mikataba kati ya mkulima mdogo na Bodi ambapo inamkodisha mkulima huyo na kazi yake ni kulima na kutunza mkong na kwamba kuna mkataba kati ya vyama vya ushirika vilivyopo katika mashamba hayo na usindikaji.
“Wote hawa wanasimamiwa na Bodi kwa kushirikiana na ofisi ya Msajili wa vyama vya ushirika Mkoa wa Tanga katika maeneo hayo TSB imekuwa ikiwasimamia wakulima kuhakikisha wanapata bei nzuri kupitia wanunuzi mbalimbali.
Kibasa ameongeza kuwa lengo la kuhamasisha kilimo hicho ni zao ambalo lina soko kubwa na ni zao ambalo linastamili magonjwa, ukame na ni la uhakika kumpatia mkulima kipato.
Bodi hiyo ni Taasisi ya serikali ambayo ipo chini wizara ya kilimo ni msimamizi na mhamasishaji maendeleo ya mkonge nchini.