Na Lucy Ngowi
DAR ES SALAAM: MKURUGENZI Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA), Profesa Joseph Ndunguru, amesema mamlaka hiyo inaendelea kuchangia ukusanyaji wa mapato ya Serikali na kulinda nchi dhidi ya uingizaji wa bidhaa zisizokidhi viwango, hususan mazao na viuatilifu hatarishi.

Amesema TPHPA imekuwa mstari wa mbele kuwezesha ufunguaji wa masoko ya mazao yanayosafirishwa nje ya nchi, sambamba na kuhakikisha mazao yanayoingia au kupita nchini hayana visumbufu kama magonjwa na wadudu waharibifu wa mazao.
Profesa Ndunguru amepongeza ushirikiano uliopo kati ya TPHPA, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na taasisi nyingine za udhibiti, hasa katika ofisi za mipakani, nchi kavu, bandari na viwanja vya ndege ambako TPHPA ina ofisi 44.
Amesema ushirikiano huo umeimarisha utekelezaji wa majukumu ya mamlaka na kuchangia kukuza uchumi wa Taifa kupitia biashara halali na salama.
Ameeleza hayo muda mfupi baada ya TPHPA kutunukiwa cheti cha kutambua mchango wake na Shirika la Forodha Duniani (WCO) katika hafla iliyoandaliwa na TRA na kufanyika katika Kumbi za Mlimani City, jijini Dar es Salaam.
Taarifa ya mamlaka hiyo imeeleza kuwa tuzo hiyo imetolewa kutokana na mchango wa TPHPA katika kulinda afya ya binadamu, mimea na mazingira dhidi ya athari za matumizi yasiyo salama ya viuatilifu, pamoja na usimamizi madhubuti wa uingizaji na usambazaji wake nchini.
TPHPA imetoa shukrani kwa WCO, TRA na wadau wote, ikiahidi kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa weledi na ufanisi kwa maslahi ya Taifa.



