Na Danson Kaijage.
DODOMA: JUMUIYA ya Maridhiano na Amani Tanzania (JMAT), imeeleza kusikitishwa na yale yanayoendelea kwenye mitandao ya kijamii hasa kwa vijana wa Kenya kumvunjia heshima Rais Samia Suluhu Hassan.
Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Shekhe Dkt. Alhad Mussa Salum, amesema hayo jijini hapa, alipokuwa akitoa tamko la taasisi hiyo kwa waandishi wa habari.
Amewaomba viongozi wa dini na wale wa kiasisa nchini Kenya kuzungumza na vijana hao kuacha kumvunjia heshima Rais Samia.
“Sisi tunaamini Kenya ina viongozi wa dini lakini kuna viongozi wa serikali tunawaomba sana tuwasihi vijana wetu hawa waone angalau heshima ya kiongozi wa Taifa jingine ikiwemo Tanzania.
“Tuwakumbushe heshima ya taifa lolote ni maadili ya watu wake kama Wakenya wataendelea na matusi ni dhahiri itakuwa ni kumkosea sana Mwenyezi Mungu kuwatukanisha wazazi wao pia na kupoteza ustarabu katika uso wa dunia kwa Taifa hilo,”amesema.
Amesema Wakenya na Watanzania bado wanahitajiana hivyo sio jambo jema linalofanywa na vijana hao.
“Tulipofika panatosha kwani moto mkubwa huanza kama cheche ndogo hivyo ipo haja ya kuzizima cheche hizi kabla haujawa moto mkubwa,”amesema.
Katika hatua nyingine amempongeza Rais Samia kwa kuonyesha ukomavu mkubwa wa kisiasa katika kadhia hiyo.
“Mama au mwanamke huzaa watoto tofauti tofauti siyo wote wanaweza kupata maadili mema lakini wote ni watoto, vijana wa Kenya ni watoto waliozaliwa na mwanamke vijana wa watanzania ni watoto waliozaliwa na mwanamke mama samehe mtoto wa mwenzio ni wako.
“Tunamkumbusha mama Samia yaliyompitia masiha Yesu mwana wa Mariam ni makubwa zaidi, lakini alisamehe saba mara sabini, aliyofanyiwa Mtume Muhammad mabaya makubwa lakini aliwaambia waliomfanyia vibaya nendeni nanyi mko huru,”amesema.
Ameipongeza Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa kutumia hekima na busara nyingi katika kuyaendea mambo mbalimbali ndani na nje ya nchi.
“Wizara na vyombo vyetu mbalimbali vya usalama vina heshima kubwa katika kumlinda mtanzania na mali zake, heshima ya viongozi wake na amani ya Tanzania kwa ujumla,”amesema.
Amesema Kenya inahitaji Amani, Tanzania inahitaji Amani hivyo wanaomba viongozi wenzao wa dini nchini humo kushirikiana katika kuwaongoza na kuwashauri vijana wao kuheshimu na kutovunja mahusiano mazuri waliyoyajenga kwa miaka mingi.