Na Lucy Ngowi
RAIS wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Dkt. Suleiman Ikomba, amesisitiza kuwa walimu wanapaswa kuepuka kutekeleza majukumu yasiyo ya taaluma yao, ili kuepuka kupata matatizo bila kujua.
Kauli hiyo imekuja baada ya walimu 17 kushikiliwa na polisi Manispaa ya Mpanda, mkoani Katavi, kuhusiana na miradi ya ujenzi wa miundombinu ya shule.
Dkt. Ikomba amesema ni muhimu kazi zisizo za walimu ziwezikwe mikononi mwa wataalamu husika ili walimu waweze kuzingatia jukumu lao kuu la kufundisha na kuchangia katika ujenzi wa taifa kupitia elimu.
“Ni muhimu kazi hizi zikaachwa kwa wataalamu husika ili walimu waweze kuzingatia zaidi taaluma waliyoisomea,” amesema, akiongeza kuwa CWT tayari imekuwa ikishauri serikali kuwasaidia walimu kuepuka majukumu yenye changamoto.
Katibu wa CWT Mkoa wa Katavi, Luya Ngonyani, akimwakilisha Katibu wa CWT Wilaya ya Mpanda, Joseph Kihwele, amesema kati ya walimu waliokamatwa, sita walitoka Shule ya Sekondari Kasokola na sita kutoka Shule ya Sekondari Rungwa. Wengine ni maofisa wa elimu wa kata na manispaa.
Kihwele amefafanua kuwa Shule ya Sekondari Rungwa ilipokea fedha za ujenzi wa mabweni mawili yenye thamani ya Sh. Milioni 21, huku Shule ya Sekondari ya Wavulana Katavi ikipokea zaidi ya Sh. Bilioni 4.1.
Walimu waliokuwa wasimamizi wa miradi hiyo walitekeleza majukumu yao kwa kufuata taratibu na miongozo iliyopo, huku miradi ikifikia hatua ya boma kwa viwango vinavyokubalika.
Walimu waliokamatwa wameachiwa kwa dhamana

