Mwandishi wetu, Arusha
TAASISI ya Wajane Tanzania (TAWIA) imeanza rasmi maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Wajane Tanzania yanayotarajiwa kufanyika Juni 23, mwaka huu 2026 mkoani Kilimanjaro, huku ikiingia ubia na Taasisi ya Wanahabari ya usaidizi wa jamii za pembezoni (MAIPAC) ili kuhakikisha tukio hilo linafanikiwa.
Akizungumza Aprili 3, 2026 katika ofisi za MAIPAC jijini Arusha, Mkurugenzi wa TAWIA, Rose Sarwatt, amesema maandalizi muhimu tayari yameanza, yakilenga kuwakutanisha zaidi ya wajane 500 kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.
Sarwatt amesema Siku ya Wajane Duniani inatambuliwa na Umoja wa Mataifa, na nchini Tanzania imekuwa ikiadhimishwa kwa ushirikiano kati ya TAWIA na Serikali.

Amebainisha kuwa maadhimisho ya kitaifa mwaka huu yatafanyika Moshi, mkoani Kilimanjaro, huku ya kimataifa yakifanyika nchini Uingereza.
“Nimekuja MAIPAC kama mmoja wa washirika muhimu wanaofanya kazi na wanawake wajane, hasa kutoka jamii za pembezoni. Ushirikiano huu ni muhimu katika kufanikisha maadhimisho haya,” amesema Sarwatt.
Ameongeza kuwa TAWIA tayari inashirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Makundi Maalum pamoja na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro, lakini bado kuna umuhimu wa kushirikisha mashirika ya kiraia (CSOs) ili kuongeza nguvu ya utekelezaji.
Katika maadhimisho ya mwaka huu, Sarwatt amesema mbali na kufanyika kwa kongamano maalum, wajane watapanda Mlima Kilimanjaro kama ishara ya ujasiri na mshikamano, huku wengine wakipata fursa ya kutembelea hifadhi za taifa.
Aidha, amewataka wadau na wafadhili kujitokeza kusaidia kufanikisha tukio hilo, akieleza kuwa ni la kihistoria na lenye lengo la kuhamasisha haki na ustawi wa wajane nchini.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa MAIPAC, Mussa Siwayombe, amesema taasisi hiyo iko tayari kushirikiana na TAWIA, akibainisha kuwa tayari imekuwa ikitekeleza miradi inayowahusisha wajane katika wilaya za Monduli, Longido na Karatu.
“Tutahakikisha tunashirikisha vyombo vya habari kwa wingi ili kuongeza uelewa wa jamii kuhusu Siku ya Wajane na masuala yanayowahusu,” amesema.
Naye Ofisa Utawala wa MAIPAC, Andrea Ngobole, amesema kupitia mtandao wa wanahabari zaidi ya 100, taasisi hiyo itatumia maadhimisho hayo kuhamasisha haki za wajane na umuhimu wa kuandika wosia ili kupunguza migogoro ya kifamilia baada ya vifo.

